Jumapili, 24 Novemba 2013

KAMPUNI YA UWINDAJI YACHOMA NYUMBA 6 ZA WANANCHI HUKO MASAGATI KILOMBERO

KAMPUNI inayomiliki kitalu cha uwindaji  ya Kilombero North Safaris katika  kata ya Masagati wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro  imelalamikiwa kuchoma moto nyumba sita za wananchi,  kuharibu  mali zilizokuwemo ndani ya nyumba hizo sambamba na kuwachapa viboko baadhi wamiliki wa nyumba hizo kwa madai kuwa wamevamia eneo lao.
 
Wananchi hao walitoa malalamiko hayo wakati wa ziara ya katibu wa CCM mkoa wa Morogoro Rojas Romuli ya  kukagua  miradi ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM pamoja na kusikiliza kero za wananchi mkoani hapa.
Diwani wa kata hiyo Blasius Makao alisema kuwa tukio hilo limetokea Octoba 27  ambapo zilichomwa nyumba 3, na octoba 28 zilichomwa nyumba 3.
‘’ Walifika watu wapatao 20 wakiwa na magari mawili katika kitongoji cha Igugu na Ipasile katika kijiji cha Ipende kata ya Masagati na kufanya uharibifu huo’’ Alisema diwani huyo.
Alisema kuwa watu hao walipofika kijijini hapo waliwachukua wajumbe wa kamati ya mazingira kwa madai ya kutaka wakawaonyeshe mipaka ya kitalu chao cha uwindaji  ambacho kipo eneo la Utengule jirani na vitongoji hivyo.
Alisema kuwa walipofika eneo la tukio wakawaambia wajumbe wa kamati hiyo ya mazingira kuwa eneo walikojenga wakazi hao ni sehemu ya kitalu chao na ndipo walipoanza kufanya uharibifu huo ambapo   wenye nyumba hizo hawakuwepo,  walikuwa wameenda katika shughuli zao za maendeleo.
Diwani huyo alisema kuwa walitoa taarifa kituo cha polisi  cha tarafa ya Milimba, polisi walifika eneo hilo na kuchukua maelezo na kwamba hakuna hatua zozote zilizochukuliwa dhidi ya wahalifu hao hadi sasa.
Pia diwani huyo alisema kuwa walifanya jitihada za kutoa taarifa kwa mbunge wa jimbo hilo Abdul Mteketa pamoja na mkuu wa wilaya hiyo Hassan Masala na kwamba viongozi hao hawakufika bali kilichofanyika ni mkuu wa wilaya hiyo kumtuma afisa tarafa wa tarafa hiyo kuangalia uharibifu huo.
Katibu wa CCM mkoa wa Morogoro Rojas Romuli aliuagiza uongozi wa CCM wilaya hiyo kuhakikisha watu hao wanafunguliwa kesi na kufikishwa mahakamani ili sheria ichukue mkondo wake.
‘’ Hatuwezi kuona watu wananyanyasika kwa stahili hii halafu tunakaa kimya, CCM ndio kimbilio la wanyonge wanaoonewa na kunyanyaswa katika  nchi hii ’’ Alisema Romuli.
Kutokana na kata hiyo ya Masagati kutokuwa na mawasiliano ya simu wananchi hao walisema kuwa wamekuwa wakishindwa kufikisha taarifa zao kwa wakati kwa viongozi husika ili hatua ziweze kuchukuliwa kwa haraka.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...