Jumapili, 24 Novemba 2013

CCM YAAGIZA WALIOFANYA UBADHILIFU KATIKA SKIMU YA UMWAGILIAJI KUCHUKULIWA HATUA.


CHAMA cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Morogoro Kimeitaka serikali kuwachukulia hatua watendaji wa idara ya kilimo  wilayani Kilombero waliohusika kufanya ubadhilifu kwa kujenga mradi wa skimu ya umwagiliaji eneo ambalo halikustahili na hivyo kuitia hasara ya shilingi milioni 700.

Katibu wa CCM mkoa wa Morogoro Rojas Romuli alisema hayo jana wakati alipotembelea katika mradi huo uliopo katika  kijiji cha Signali kata ya Kiberege wilayani Kilombero, akiwa katika ziara yake ya kukagua utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
Romuli alisema kuwa kwa mradi mkubwa kama huo ni lazima ungefanyika utafiti wa kina ili kubaini kama eneo hilo linafaa kwa ajili ya ujenzi wa mradi huo, kwa kuzingatia upatikanaji wa maji ya uhakika.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Kiberege ulipojengwa mradi huo, Ramadhani Makung’uto  alisema kuwa mradi huo ulipowasilishwa katika baraza la madiwani la halmashauri ya wilaya hiyo waliukataa kutokana na kwamba walijua hautakuwa na tija kwa sababu eneo hilo halina maji kwa muda wote kama ambavyo inastahili kwa mradi wa aina hii.
‘’ Mradi huu madiwani walikukataa, kilichotokea ni kwamba wataalamu wa kilimo wa kanda ndio waliolazimisha mradi ukajengwa katika eneo hilo na sasa hauna tija. Kwa mradi huu fedha za wananchi zimepotea bure’’ Alisema.
Wataalamu hao wametajwa kuwa ni Injinia Joshi Chum na mwingine aliyetambulika kwa jina moja la Injinia Mlelwa kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro.
Mwenyekiti CCM wilaya ya Kilombero Abdalla Kambangwa  alisema kuwa aliyekuwa  Afisa maendeleo ya   kilimo  na mifugo Mary Kitua ambaye kwa sasa amehamishiwa wilaya ya Ngorongoro ndiye aliyehusika na usimamizi wa mradi huu na amekwamisha miradi mingine mingi mingi katika wilaya hiyo ikiwemo  ya umwagiliaji , majosho, maghala ya kuhifadhia mazao pamoja na masoko.
‘’ Katika miradi mingi ambayo tumeitembelea tumebaini imekwama, na kila mwaka katika bajeti zinaonyesha kuna fedha zimetengwa kwaajili ya miradi kama hiyo ambayo haikamiliki’’.
Mwenyekiti huyo alisema kuwa ukaguzi wa fedha za miradi hiyo ulishafanyika na kwamba hadi sasa bado ripoti haijatolewa jambo ambalo wananchi wanalilalamikia.
Katibu wa CCM wa Mkoa wa Morogoro Rojas Romuli ametaka hatua zichukuliwe dhidi ya Afisa aliyefanya ubadhilifu wa mamilioni ya fedha za miradi ya kilimo na mifugo katika wilaya hiyo ambaye kwa sasa amehamishwa katika wilaya nyingine jambo ambalo sio sahihi, na kwamba inafaa awajibishwe.
Pia ametaka hatua zichukuliwe dhidi ya wataalamu waliolazimisha mradi huo kujengwa katika eneo ambalo halistahili na kusababisha upotevu mkubwa wa fedha za umma.
Mwisho
 
 
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...