Jumanne, 11 Machi 2014

MVOMERO WATAKA MASHAMBA PORI 50 YAREJESHWE KWA WANANCHI

MAKALA maalumu ya migogoro ya ardhi  wilayani Mvomero.
WILAYA ya Mvomero ni miongoni mwa wilaya zinazokabiliwa na migogoro ya wakulima na wafugaji iliyoduma kwa muda mrefu hapa nchini.


Migogoro hiyo imekuwa ikisababisha maafa ikiwemo mali kuharibiwa na wakati mwingine vifo na baadhi ya wananchi kujeruhiwa vibaya.


Kwa Mvomero changamoto hiyo inasababishwa na ufinyu wa eneo la ardhi na mgawanyo wa matumizi bora ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji.


Wilaya hiyo miongoni mwa wilaya sita za mkoa wa Morogoro, wakazi wake kwa asilimia kubwa wanajishughulisha  na kilimo.Ina ukubwa wa kilometa za mraba 7,325 ambalo ni sawa na Hekta 732,500.


Kwa mujibu wa takwimu za sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 wilaya hiyo ina wakazi wapatao 312,109 kati yao wanaume ni 154,843 na wanawake ni 157,266.

Kulingana na takwimu za sensa, wilaya hiyo ina wafugaji wapatao 18,749  wanaomiliki ng’ombe wa asili 138,396  na  ng’ombe wa maziwa 10,744.


Mifugo mingine ni mbuzi 74,547, kondoo 20,459, Wakati eneo linalofaa kwa ufugaji ni hekta  266,400 sawa na ekari 676,656.


Hata hivyo kwa mujibu wa wataalamu eneo ng’ombe mmoja huitaji ekari 10 za malisho kwa mwaka na kwamba eneo hili linatosha ng’ombe 67,666 ambapo mbuzi kondoo hawatakuwa na eneo la malisho.


Kwa upande wa kilimo takwimu zinaonyesha licha ya asilimia 82 ya wakazi kufanya shughuli za kilimo lakini asilimia saba hufanya biashara na asilimia moja  ufugaji huku wengine asilimia 10 wakifanya kazi mbalimbali.


Hata hivyo shughuli za kilimo zinafanywa katika eneo dogo la wilaya hiyo. Kati ya Kilometa za mraba 549,379 zinazofaa kwa kilimo , zinazotumika ni hekta 247, 219 ambazo  ni sawa na asilimia 45.


Pia eneo linalofaa kwa kilimo ni hekta ambapo eneo linalolimwa ni wastani wa hekta ambazo ni sawa na asilimia 45 ya eneo lote.



Hata hivyo kumekuwa na idadi kubwa ya mifugo na kwamba imekuwa ikibadilika  mara kwa mara kutokana na ufugaji wa kuhamahama hasa wakati wa kiangazi ambapo  wafugaji huamisha mifugo kufuata maji na malisho.


Tatizo la ufinyu wa ardhi linatajwa na Mkuu  wa wilaya ya Mvomero, Antoni Mtaka kuwa ni tatizo linalosababisha migogoro hiyo.

Mbali na uhaba wa ardhi pia kuna tatizo la kutozingatia mgawanyo wa ardhi inayotengwa kwa kazi fulani.


Ni kutokana na migogoro hiyo iliyoduma kwa muda mrefu Mtaka alisema wameanzisha kauli mbiu isemayo “

Ardhi haiongezeki watumiaji wa ardhi wanaongezeka’’.


Mtaka alisema kutokana na migogoro hiyo inayotokana na ufinyu wa ardhi, wilaya imeandika barua kwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera, kuomba kufutwa kwa mashamba pori yapatayo 50  yaliyotelekezwa ili yagawiwe kwa wananchi.


‘’ Endapo mashamba hayo yatarudishwa na kugawiwa kwa wananchi itasaidia kupunguza migogoro ambayo chanzo chake kikubwa ni kukosekana kwa ardhi na hivyo wakulima na wafugaji kugombea ardhi hiyo finyu’’ anafafanua .


Kutokana na hilo Mtaka alisema Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi imeunda kikosi kazi ambacho kinasaidia upimaji wa ardhi katika wilaya hiyo ili kuweza kubaini mipaka ya vijiji vyote 115 vilivyopo katika  kata 23 za tafara 4 za wilaya hiyo.


Kwa mujibu wa sheria ya ardhi kifungu cha 3, ardhi yote ya Tanzania  ni mali ya  umma na kwamba Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ndiye mwenye mamlaka kwa niaba ya Watanzania  wote.


Na kulingana na sheria hiyo Rais ndiye mwenye uwezo wa kufuta umiliki wa ardhi pale anapoona inafaa kufanya hivyo kwa manufaa ya umma.


Hivi karibuni  mapema mwezi Januari Naibu Waziri wa Ardhi, George Simbachawene aliahidi mbele ya viongozi wa wilaya hiyo kuwa endapo migogoro hiyo haitapata suluhu katika kipindi hiki wizara yake ilivyoounda kikosi kazi hicho cha upimaji wa ardhi yuko tayari kujiuzuru.


‘’ Kama migogoro hii ya ardhi haitafikia tamati, niko tayari kujiuzuru nafasi yangu hii, siko  tayari kuona migogoro hii ikiendelea na kusababisha uvunjifu wa amani, watu kupoteza mali zao na hata maisha,” ni kauli ya Simbachawene.


Naye Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Kaika Saning’o Telele,   Februari 21 alipotembelea wilaya ya Mvomero alisema ‘’ tayari tuna migogoro ya ardhi ya kutosha hatuitaji migogoro mingine,’’ alisema.


Kwa mujibu mara nyingi migogoro hiyo inatokana na ugawaji wa ardhi usiozingatia matumizi bora ya ardhi na na kwamba mara nyingi wamekuwa wakipewa wawekezaji maeneo hata ya wafugaji na hivyo wafugaji kukosa maeneo na kuanza kugombania kwa  na wakulima.


‘’  Maeneo ya wafugaji anapewa mwekezaji anajenga hotel wafugaji wanaogea na mara nyingine hata kuingia katika hifadhi na hivyo kusababisha migogoro hiyo’’ alisema.


Musa Rajabu mkazi wa  Turiani wilayani Mvomero alisema kuwa imefika wakati sasa kuangalia uwezekano wa kutengua hatimiliki za mashamba pori na kuwagawia wananchi kwa kuwatenganisha wakulima na mafugaji ili kuepusha migogoro.


‘’ Ili migogoro iweze kupata suluhu hakuna budi kwa serikali kuangalia uwezekano wa kutwaa mashamba hayo yasiotumika kwa miaka mingi sasa ili kuwapatia wananchi kuweza kuyatumia kwa shughuli za kibinadamu,’’ alisema.


Rehema Juma mkazi wa  kijiji cha Mkindo wilayani humo alisema kuwa migogoro hiyo pamoja na kuwepo kwa ufunyu wa ardhi lakini pia umekuwa ukichangiwa kwa kiasi kikubwa na baadhi ya wenyeviri wa vitongoji na vijiji kuwakaribisha wafugaji wageni kinyemela .


Alisema kuwa pia kumekuwa na tabia kwa  wafugaji wazawa kuwakaribisha wafugaji wavamizi kimya kimya na kwamba wanapokuja wanakuja bila mifugo na kusoma ramani kisha kufuta mifugo yao na hali hiyo imekuwa ikichangia kwa kiasi kikubwa migogoro hiyo.


Kwa upande wake Mbunge wa  Morogoro Kusini, ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM mkoa wa Morogoro, Inocent Kalogiries katika kikao cha kamati ya ushauri ya mkoa kilichofanyika mapema mwezi Januari alisema kuwa mbali na kuomba mashamba pori hayo kufutiwa umiliki wake lakini pia mkoa wa Morogoro kwa sasa hawahitaji wafugaji.


‘’Mkoa wa Morogoro ni mkoa wa kilimo sasa hawa wafugaji wanatoka wapi, kwanini tunawafumbia macho, ni lazima tuchukue hatua,’’ Alisema.


Naye Mkurugenzi wa  Kituo cha Msaada wa Sheria, Frola Masoy alisema  wilaya ya Mvomero ni moja ya wilaya ambayo walifanyia utafiti juu ya migogoro hiyo na kuamua kutoa elimu kwa wananchi wake kwaajili ya kumiliki ardhi.


Alisema wananchi hao walifundishwa jinsi ya kujiandisha na kuomba hatimiliki za kimila ili kuweza kumiliki kihalali na kuondokana na migogoro isiokuwa ya lazima na kwamba kuweza kuzitumia katika kupata mikopo kwa lengo la kujikwamua kiuchumi.


‘’ Tumewafundisha  wajue kuwa ardhi inaweza kumilikiwa kimila na badae kuomba hatimiliki za kudumu, sambamba na umilikaji wa pamoja kwa maana ya mume na mke,’’ Alisema.


Alisema kuwa umiliki wa pamoja wa ardhi umekuwa ukisaidia pia kuondokana na migogoro ya ardhi  katika familia na kwamba mara nyingi mwanaume anapomiliki ardhi peke yao imekuwa ikisababisha migogoro mingi  pale anapofariki dunia na ndugu wa mwanaume kuamua kutwaa mali za ndugu yao.


Viongozi wa wilaya hiyo akiwemo mkurugenzi, wakuu wa idara wa halimashauri , na mwenyekiti wa halmashauri hiyo , viongozi wa chama cha Mapinduzi wilaya hiyo, kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya walifanya ziara  ambapo walikutana na wenyeviti wa vitongoji 640 wenyeviti na watendaji wa vijiji 115, watendaji wa kata 23 pamoja na madiwani wote na maafisa tarafa 4 kwa lengo la kutoa maelekezo juu ya kutatua migogoro hiyo.


Katika maelekezo hayo wananchi walitakiwa kutouza maeneo yao hovyo pamoja na kutoingiza wafugaji kiholela  na kujenga tabia ya kuwa na vikao vya ujirani mwema mara kwa mara ili kutatua migogoro inapokuwa katika hatua za awali badala  ya kusubiri inapokuwa katika hatua mbaya hali inayofanya kutumia nguvu kubwa kutatua.



Pia viongozi hao waliwataka wafugaji wavamizi kuondoka nje ya wilaya hiyo na kurudi maeneo waliotoka ili kupunguza wingi wa mifugo na uharibifu wa mashamba  wa makusudi  kutokana na utafiti uliobaini kuwa wafugaji hao wavamizi huvamia mashamba ya wakulima nyakati za usiku na kulisha mifugo yao katika mashamba hayo.


Pamoja na mambo mengine uongozi huo ulisitisha shughuli zote za ulinzi wa jadi na badala yake shughuli zote za ulinzi zitafanywa na jeshi la polisi, hatua hiyo ilikuja baada ya kuwepo kwa vijana waliounda kikundi cha asili kijulikanacho kama Mwano ambacho kilitoka katika kundi la wakulima kilichokuwa na kazi ya kukamata ng’ombe na kuwashikilia kisha kutoza fedha kama fidia kwa mfugaji atakayeonekana kuingiza ngombe wake katika mashamba ya wakulima.


Zoezi hilo la kikundi hicho lilichangia kwa kiasi kikubwa mapigano baina ya wakulima na wafugaji hasa pale wanapokamata ng’ombe na kutoza faini hata kama mfugaji akiamua kufanya makubaliano na mkulima mwenyewe na hivyo kusababisha wakulima nao  kutumia silaha za moto kuwadhibiti kundi hilo ambalo mara zote limekuwa likitumia silaha za jadi.


Kamanda wa polisi mkoa wa Morogoro Faustine Shilogile alisema kuwa kamati ya ulinzi na usalama iliamua kusitisha shughuli hizo za ulinzi kwa kundi hilo kutokana na kutokea madhara makubwa Novemba mwaka jana ambapo vijana hao walizuia ng’ombe wa  200 wanaomilikiwa na Semwako Matunda baada ya ng’ombe zake kuingia katika mashamba ya wakulima  4 katika kijiji cha Hembeti wilayani humo.


Kamanda huyo anaelezea tukio hilo kuwa wakulima hao walikamata ng’ombe hao na kupeleka katika ofisi ya kijiji  ili kupzta muafaka wa uharibifu huo katika mashamba yao na kwamba ofisi ya kijiji ilimwita mfugaji huyo  ili kupata muafaka wa tatizo hilo ambapo wakulima walimtaka mfugaji huyo  kulipa kiasi cha shilingi milioni 3 kitu ambacho mfugaji huyo hakuridhia  na kuwataka wakulima hao kupeleka suala hilo polisi.



Alisema kuwa kundi hilo la mwano ambalo tayari lilishapigwa marufuku shughuli hizo walikataa na kuendelea kuwashikilia ng’ombe hao  ambapo ilipofika Novemba 5 mmiliki wa ng’ombe huyo na vijana kadhaa wa Morani walifika katikan ofisi hiyo ya kijiji  ambapo ng’ombe hao walikuwa chini ya ulinzi  na kuwataka kutoa mifugo hiyo kitendo ambacho hakikufikiwa muafaka na kundi hilo na hivyo  kuanza mapigano baina ya pande hizo mbili.


Alisema kuwa madhara yaliotokea katika mapigano hayo  watu sita walifariki dunia huku wengine 35 kujeruhiwa  sambamba na wananchi wa  vijiji vya Hembeti, Dihombo, Msufini na Mkindo walifanyiwa uharibifu wa mali zao kwa kuchomewa nyumba zao moto, kuibiwa chakula kilichokuwa majumbani mwao pamoja na kupotea mifugo iliokuwa majumbani mwao.
Tatizo hilo lilisababisha kuathiri shughuli za kiuchumi  na kijamii maeneo hayo kutokana na wananchi kushindwa kufanya shughuli zao kutokana na mapigano hayo kwa kuhofia usalama wao.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...